Waziri wa Utumishi wa Umma Geoffrey Ruku, ametangaza mikakati kabambe inayolenga kulainisha taratibu za ununuzi katika Huduma ya Taifa kwa Vijana (NYS).
Waziri huyo aliyasema hayo leo Ijumaa afisini mwake katika jumba la Harambee, baada ya mkutano wa mashauri na maafisa wa wizara yake, Halmashauri ya kudhibiti shughuli za Ununuzi wa Umma (PPRA) na wale wa NYS.
Hatua hii inajiri kufuati madai ya ufujaji wa shilingi bilioni mbili katika Taasisi ya NYS tawi la Gilgil, kuambatana na ripoti ya Tume ya Maadili na Kukabiliana na Ufisadi EACC ya May 7, 2025.
Ruku aliagiza PPRA kuanzisha uchunguzi mara moja katika taratibu zote za ununuzi na utupaji bidhaa za huduma ya NYS kunzia mwezi Julai mwaka 2019 hadi leo.
“Vijana wa taifa hili wanahitaji huduma ambazo ni wazi na zinazowajibishwa. Ukiukaji wowote wa katiba hautakubaliwa,” alisema Waziri Ruku.
Aidha, waziri huyo alitaaka taasisi husika kuwahoji wanaoshukiwa kuhusika katika sakata hiyo na kuwaondoa watakaopatikana na hatia katika shughuli za ununuzi wa umma.