Takriban watu 40 wameuawa katika shambulizi dhidi ya kambi ya watu waliokimbia makazi yao, katika jimbo la Darfur magharibi mwa Sudan, kulingana na kundi la misaada linalofanya kazi katika eneo hilo.
Kitengo cha Kukabiliana na Dharura kinasema shambulio la Jumatatu lilitekelezwa na Rapid Support Forces (RSF). Kamati ya upinzani katika mji wa karibu wa el-Fasher, inayoundwa na wananchi wa eneo hilo na wanaharakati, pia iliripoti tukio hilo.
El-Fasher, mji ulioshambuliwa vikali pia, ni eneo la mwisho huko Darfur kwa jeshi na washirika wake, ambao wamekuwa wakipigana na wanamgambo wa RSF katika vita vya wenyewe kwa wenyewe vya miaka miwili.
Mgogoro huo umesababisha mgogoro wa kibinadamu huku Umoja wa Mataifa ukionya kwamba familia zilizokwama katika mji huo uliozingirwa zinakabiliwa na njaa.
Kundi la misaada ya ndani la Abu Shouk, ambako takriban watu 200,000 wanaishi, lilisema baadhi ya waliouawa katika shambulio hilo walipigwa risasi wakiwa majumbani mwao huku wengine wakipigwa risasi hadharani.
Shirika lenye makao yake makuu nchini Marekani linalochambua picha za satelaiti na video linasema kundi kubwa la magari 40 yalionekana katika vitongoji vya kaskazini-magharibi mwa kambi hiyo, ripoti inayothibitisha shambulio hilo lilitoka kaskazini.
RSF imekuwa ikishutumiwa pakubwa kwa mauaji ya kikabila huko Darfur wakati wa vita hivi. RSF imekanusha tuhuma hizo.
Kambi za watu waliokimbia makazi yao karibu na El-Fasher mara nyingi zimekuwa zikishambuliwa wakati wa vita.
Aprili, zaidi ya watu 100 walikufa na maelfu walikimbia kambi ya Zamzam wakati RSF ilipoikali na kuichukua.
Tangu mzozo huo uanze Aprili 2023, maelfu ya watu wamekufa, milioni 12 wamelazimika kutoka makwao na njaa imetangazwa katika sehemu za nchi.