Kuanzia Machi 23 hadi 31, vijana wanne wa kujitolea kutoka Manispaa ya Chongqing nchini China, walishiriki katika mpango wa siku nane wa kimataifa wa kutunza ikolojia nchini Kenya.
Mpango huu, ulioandaliwa na wakfu wa mawasiliano ya kimataifa wa Chongqing Luhai na kituo cha kubadilishana utamaduni cha Asia-America-Uropa, kwa msaada wa mfuko maalum wa huduma ya kujitolea wa Chongqing Luhai, ulikusudia kukuza maelewano ya kitamaduni na ushirikiano wa kimazingira kati ya vijana wa Kichina na wa Kiafrika.
Maono ya pamoja
Safari hiyo ilianza katika Makavazi ya Kitaifa ya Kenya, ambapo wanafunzi walipata ufahamu kuhusu utofauti wa viumbe vya nchi hiyo kupitia maonyesho na sampuli. Li Xincan, ambaye ni mwanafunzi wa darasa la sita kutoka Shule ya Msingi ya Honghe katika Wilaya ya Yongchuan ya Chongqing, alionyesha mshangao mkubwa kuhusu wanyama wa porini wa Afrika, akisema, “Kuona sampuli za tembo wa Kiafrika kuliinua ufahamu wangu kuhusu ukubwa wao—ni wakubwa zaidi kuliko tembo wa Asia!”
Kikundi hicho kisha kilitembelea makao makuu ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Mazingira (UNEP) jijini Nairobi, ambapo walipata ufahamu kuhusu sera za kimataifa za mazingira na juhudi za ushirikiano katika masuala ya uhifadhi.
Ubadilishanaji wa tamaduni
Kilele cha safari hiyo lilikuwa tukio la mkutano wa kubadilishana kwa ustaarabu wa ikolojia kati ya China na Afrika ulioandaliwa katika Taasisi ya Confucius ya Chuo Kikuu cha Nairobi. Wanafunzi kutoka manispaa ya Chongqing walichukua nafasi muhimu. Li Meile, mwanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Xiamen nchini Malaysia, alikusanya maonyesho ya picha yenye kichwa “Jiji la Tai,” ikionyesha juhudi za uhifadhi wa ndege wa rapa huko Chongqing.
Wakati huo huo, Yang Yunqiao, mwanafunzi wa shule ya upili kutoka Shule ya Upili ya Reli ya Chongqing, alifanya mahojiano na wageni wa kimataifa kuhusu utunzi wa ikolojia na jinsi shughuli hiyo inavyotekelezwa nchini China na barani Afrika.
Wawakilishi hao pia walishirikiana kuandika na kuzindua “Mpango wa Kijani wa Vijana wa China na Afrika,” na kutangaza kujitolea kwao kuendeleza mbinu na kukuza maendeleo endelevu katika sekta hiyo.
Jin Shishuang, mwanafunzi wa Kenya katika Taasisi ya Confucius, alisema, “Hii si ziara tu—ni mwanzo wa ushirikiano wa muda mrefu kati ya vijana wetu.”

Katika mbuga ya Wanyama ya Masai Mara, vijana hao wa kujitolea walishirikiana na wanafunzi wa eneo hilo, wakishiriki hadithi za utofauti wa viumbe wa Chongqing kupitia alama za “Jiji la Tai.” Kiongozi mmoja wa kijamii, Simon Masago, alikaribisha ushirikiano zaidi akisema, “Tungependa kuona vijana zaidi wa Kichina wakijiunga na miradi kama hii, kwa mfano kujenga uzio, kupanda bustani, na kuboresha maisha.”
Hatua ya maendeleo endelevu
Mkurugenzi wa kituo cha kubadilishana utamaduni cha Asia-America-Uropa, Li Hui, alisisitiza dhamira pana ya mpango huo, akisema, “Tunataka vijana kuungana kwa kina—sio tu kwa mambo ya utamaduni, bali pia kwa hisia.”
Safari hii ya kwanza chini ya mradi wa “huduma ya kujitolea ya kimataifa ya ardhi-M baharini” inatarajiwa kupanuka, na kuwezesha ubadilishanaji zaidi katika maeneo mengine ya Afrika.
Chen Can, naibu katibu mkuu wa wakfu wa mawasiliano ya kimataifa wa Chongqing Luhai, aliongeza kusema, “Huduma halisi ya kimataifa inamaanisha kujiingiza katika jamii za ndani. Tutazidi kuwapa vijana uwezo wa kujifunza, kukua, na kuchangia katika maendeleo endelevu ya kimataifa.”
Wakati mabalozi hawa vijana wanaporejea nyumbani, uzoefu wao unasimama kama ushahidi wa nguvu ya ushirikiano wa mipaka katika kuimarisha mustakabali wa sayari yetu.