Mabingwa mara mbili wa kombe la CHAN Morocco, wamefufua matumaini ya kufuzu kwa robo fainali katika makala ya mwaka huu baada ya kuwalaza Zambia mabao 3-1, katika mchuano wa tatu wa kundi A uliosakatwa Alhamisi jioni uwanjani Nyayo.
Nahodha Mohamed Hrimat aliwaweka Atlas Lions uongozini katika dakika ya mwisho ya nyongeza ya kipindi cha kwanza, kabla ya Oussama Lamlioui kuongeza la pili dakika ya 67.
Andrew Phiri alikomba moja kwa Chipolopolo dakika tatu baadaye, kisha Sabir Bougrine, akapachika goli la tatu katika muda wa nyongeza.
Ushindi huo unaichupisha Morocco hadi nafasi ya pili kwa alama sita, pointi moja nyuma ya Kenya.
Simba wa Atlas watafunga ratiba ya kundi hilo Jumapili dhidi ya DR Congo.
Kenya itafunga ratiba dhidi ya Zambia.