Sasa ni rasmi kwamba Katibu Mkuu wa Chama cha Wauguzi nchini (KNUN) Seth Panyako atawania ubunge katika uchaguzi mdogo katika eneo bunge la Malava kwa tiketi ya chama cha DAP-K.
Chama hicho kinachoongozwa na Waziri wa zamani wa Ulinzi Eugene Wamalwa kilimkabidhi Panyako cheti cha uteuzi leo Alhamisi wakati wa hafla iliyofanyika katika makao makuu ya chama hicho jijini Nairobi.
Hata hivyo, kumekuwa na uvumi kwamba Panyako huenda akazuiliwa kuwania wadhifa huo kwani alikawia kujiuzulu kama mwanachama wa Bodi ya Hazina ya Serikali za Kaunti (LAPFUND).
Huku madai hayo yakikolea, wengi wanasubiri kuona ikiwa Panyako atapata idhini ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kuwania wadhifa huo.
Vyama vingine, kikiwemo chama tawala cha UDA, bado vinapanga mikakati ya namna ya kutwaa kiti hicho kilichoachwa wazi kufuatia kifo cha aliyekuwa mjumbe wa eneo bunge hilo Malulu Injendi mapema mwaka huu.
IEBC imepanga kuandaa chaguzi ndogo katika maeneo bunge 24 Novemba 27, ikiwemo Malava.