Rais William Ruto amemshukuru Rais Donald Trump wa Marekani na serikali yake kwa kile alichotaja kuwa ukarimu na mashauriano ya kufana ambayo yamefungua ukurasa mpya wa ushirikiano kati ya nchi hizi mbili.
Kwenye taarifa , Rais Ruto alisema mashauriano ya ngazi za juu kati ya nchi hizi mbili mjini Washington, DC, ni hatua kubwa ya kuimarisha zaidi uhusiano kati ya Kenya na Marekani.
Rais Ruto alisema Kenya inafurahia kujitolea na moyo wa ushirikiano wa serikali ya Trump katika kushughulikia masuala mbali mbali.
“Kwa niaba ya serikali na raia wa Kenya, namshukuru Rais Donald Trump na Serikali ya Marekani kwa ukarimu walioonyesha kwa ujumbe wa Kenya Jijini Washingtona DC,” alisema Rais Ruto.
Kuhusu afya, Rais Ruto alisema Kenya inafurahia ushirikiano mpya uliopo kati ya nchi hizi mbili katika kuchunguza kuenea kwa magonjwa,kuimarisha afya ya kimsingi na kurahisisha upatikanaji wa teknolojia ya matibabu.
Rais Ruto aliipongeza Marekani kwa msaada wake wa kuleta uthabiti katika upembe wa Afrika na eneo la maziwa makuu.
Kiongozi wa taifa alisema mashauriano yao kuhusu mbinu za kukabiliana na ugaidi, usalama wa majini na juhudi za kusuluhisha mizozo yalikuwa ya kufana na kutoa hakikisho kwamba wakati Kenya na Marekani zinapochukua hatua za pamoja,eneo hili huwa thabiti.