Kiongozi wa chama cha Orange Democratic Movement – ODM Oburu Oginga, amemteua mwanadiplomasia wa hadhi ya juu Dkt. Renish Achieng Omullo kuwa mshauri wake wa masuala ya kikanda na kimataifa.
Hatua hiyo inaashiria juhudi za chama hicho za kuimarisha msimamo wake kimataifa na kuboresha sura yake nje ya mipaka ya Kenya.
Uteuzi huo ni sehemu ya jitihada za Oburu kuunda kundi litakalompa msaada unaohitajika ili kutoa uongozi madhubuti ndani ya chama.
Akimsifu Omullo kama mtu anayefaa kwa wadhifa huo, Oburu alibainisha kuwa ana nafasi ya kipekee ya kutoa mchango muhimu utakaopanua ushawishi wa chama duniani na kuimarisha uaminifu wake katika jukwaa la kimataifa.
Omullo ni mwanadiplomasia mwenye uzoefu mkubwa na msingi imara katika ushirikiano wa mipakani, biashara ya kimataifa na diplomasia.
Akiwa na uelewa wa kina wa masuala ya kimataifa unaoungwa mkono na uzoefu wa ngazi ya juu, anakuja na maarifa na weledi utakaosaidia kuimarisha ushirikiano wa nje wa chama na kuinua hadhi yake katika majukwaa ya kimataifa.
Kazi yake iliyopambwa na mafanikio inajumuisha kuteuliwa na Rais wa Sudan Kusini, Salva Kiir kuwa mjumbe maalum kwenda Ujerumani, akiwa na makazi yake mjini Berlin.