Ndege ya kivita ya India imeanguka ilipokuwa ikifanya maonyesho katika anga la Dubai na rubani mmoja akapoteza maisha, maafisa wamesema.
Jeshi la Wanahewa la India lilisema katika taarifa: “IAF inajutia sana kupoteza maisha na inasimama pamoja na familia iliyofiwa katika wakati huu wa huzuni.
“Mahakama ya uchunguzi inaundwa, ili kubaini chanzo cha ajali.”
Ndege ya Hindustan Aeronautics Ltds Tejas ilianguka takriban 14:10 saa za eneo (10:10 GMT), kulingana na Associated Press.
Ofisi ya Vyombo vya Habari ya Dubai na Wizara ya Ulinzi ya UAE zimesema wazima moto na huduma za dharura “walijibu haraka” tukio hilo.
Picha za video za ajali hiyo zinaonyesha moshi mweusi ukipanda angani.
Tovuti ya Dubai Airshow 2025 inasema hafla hiyo imevutia zaidi ya wahudhuriaji na waonyeshaji 148,000 kutoka kampuni 1,500.
Ajali hiyo mbaya ilitokea siku ya mwisho ya onyesho la anga lililoanza Jumatatu, lililoandaliwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Al Maktoum.