Jeneza la wazi la Papa Francis limehamishiwa katika Kanisa la St. Peter’s Basilica kwa siku tatu, huku maelfu ya watu wakikusanyika kutoa heshima zao kwa kiongozi wa Wakatoliki duniani.
Kengele za Basilica hiyo zililia wakati jeneza la mbao liliposafirishwa kwa maandamano mbele ya umati uliokuwa umejaa katika Uwanja wa St. Peter’s Basilica, likisindikizwa na makadinali waliovaa mavazi mekundu na Walinzi wa Uswisi wa Vatican.
Mahujaji na watalii walikuwa wakipiga picha, huku baadhi wakipiga makofi wakati maandamano yalipopita kutoka makaazi ya Santa Marta, ambako Papa huyo mwenye miaka 88 alifariki Jumatatu baada ya kupata kiharusi.
Mwili wa Francis ulikuwa umehifadhiwa katika kanisa la Santa Marta, alikokuwa akiishi wakati wote wa miaka 12 ya upapa wake, lakini sasa utalala wazi kwa heshima katika basilika hiyo hadi mazishi Jumamosi.
Mazishi yanatarajiwa kuvutia maelfu ya mahujaji na viongozi wa kimataifa, akiwemo Rais wa Marekani Donald Trump, Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky, na Mwanamfalme William wa Uingereza.