Msongo wa mawazo walaumiwa kama chanzo cha mauaji na kujitoa uhai

Marion Bosire
2 Min Read

Kufuatia ongezeko la visa vya kujitoa uhai na mauaji vinavyohusishwa na matatizo ya afya ya akili, makasisi na viongozi wametoa wito kwa serikali kupunguza gharama ya maisha.

Wameitaka serikali pia kuanzisha vituo zaidi vya ushauri nasaha kama njia ya kukabiliana na mzozo huu unaozidi kuongezeka.

Wakiongozwa na Askofu Samuel Kamau, mlezi wa Kanisa la AIPCEA eneo la Gatundu ya kati, makasisi hao walieleza kuwa mzozo huu wa afya ya akili unasababishwa na gharama ya juu ya maisha na ukosefu wa ajira.

Askofu Kamau alizihimiza makanisa kuongeza juhudi kwa kuandaa semina zaidi za ushauri nasaha na maombi, hasa kwa wanandoa wachanga, ili kuwasaidia kupata nguvu na kukabiliana na changamoto za maisha kwa matumaini na uvumilivu.

Aidha, alihimiza vijana wasikate tamaa wanapokumbwa na changamoto, bali wajitahidi kutumia kila fursa waliyonayo kupata riziki halali kwa bidii na kujituma.

Kauli zake ziliungwa mkono na aliyekuwa Naibu Gavana wa Kaunti ya Kiambu, Bi. Joyce Wanjiku Ngugi, aliyetoa wito kwa serikali kuunda nafasi zaidi za ajira ili kusaidia vijana wasio na shughuli kupata kipato na kurejesha matumaini yao ya maisha.

Bi. Wanjiku aliongeza kuwa kuna umuhimu wa kuwawezesha wataalamu na vituo vya ushauri nasaha ili kutoa msaada wa kitaalamu kwa wale wanaokumbwa na msongo wa akili.

Alisisitiza haja ya hatua za mapema, akipendekeza waathirika wa dawa za kulevya wapatiwe huduma za marekebisho na wengine wapatiwe ushauri ili kuzuia matukio ya kujitoa uhai na tabia hatarishi.

Walizungumza wakati wa Ibada ya Upya wa Nadhiri za Kanisa iliyofanyika katika Kanisa la AIPCEA Gatundu North, Kaunti ya Kiambu.

Share This Article