Maafisa wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) wamemkamata aliyekuwa mbunge wa Baringo Central Sammy Mwaita kwa tuhuma za unyakuzi wa ardhi jijini Nairobi.
Mwaita, ambaye pia aliwahi kuhudumu kama Kamishna wa Ardhi, alikamatwa siku ya Jumapili katika eneo la Kilimani.
Anatarajiwa kufunguliwa mashtaka ya kupanga kutekeleza uhalifu, kubuni stakabadhi bila idhini, utumizi mbaya wa mamlaka na kutoa habari za kupotosha kwa afisa wa umma.
Kupitia ukurasa wa X, DCI ilisema kukamatwa kwake kulijiri baada ya maagizo ya Kiongozi wa Mashtaka ya Umma kuhusu vipande viwili vya ardhi vya thamani ya mamilioni ya pesa.
“Kwa sasa Mwaita anazuiliwa na maafisa wa polisi, akisubiri kufikishwa mahakamani, huku washirika wake wakiendelea kutafutwa,” ilisema DCI kwenye taarifa.