Klabu ya Mara Sugar ndiyo timu ya kwanza kupandishwa ngazi kushiriki ligi kuu ya FKF msimu ujao baada ya kuikung’uta Silibwet Leons mabao 4-0, katika mchuano wa Jumamosi uwanjani Awendo Green kaunti ya Migori.
Mara Sugar ndiyo timu ya kwanza kutoka jamii ya Maa iliyo katika kaunti za Narok na Kajiado kufuzu kushiriki ligi kuu ya FKF, kuanzia msimu ujao wa mwaka 2024/2025.
Klabu hiyo yenye makao yake kijijini Enoosaen eneo la Trans Mara, imekuwa ikichezea mechi zake za nyumbani katika uwanja wa Migori na inaongoza jedwali kwa alama 78, zikisalia mechi tatu msimu ukamilike huku Mathare United wanaokalia nafasi ya pili wakiihitaji tu sare ili kurejea ligini.