Mahakama ya upeo nchini Israel imesema katika uamuzi usio wa kawaida kwamba serikali ya Israel inanyima wafungwa wapalestina chakula maksudi huku vita vinavyochukuliwa kuwa mauaji ya halaiki vikiendelea Gaza.
Jopo la majaji watatu ambalo limejizuia kuchukua hatua dhidi ya serikali au jeshi katika miezi 23 ya vita vya Gaza, lilitoa uamuzi huo kufuatia ombi la makundi mawili ya kutetea haki ya Israel.
Mahakama ilitoa uamuzi kwa kauli moja Jumapili kwamba serikali ya Israeli ina wajibu wa kisheria kuwapatia wafungwa wa Kipalestina milo mitatu kwa siku ili kuhakikisha “kiwango cha chini cha maisha” na ikaamuru mamlaka kutimiza wajibu huo.
Katika uamuzi wa kura mbili dhidi ya moja, mahakama pia ilikubali ombi lililowasilishwa mwaka jana na Jumuiya ya Haki za Kiraia nchini Israeli (ACRI) pamoja na Gisha, na kuunga mkono madai yao kwamba serikali imekuwa ikidhibiti kwa makusudi chakula cha wafungwa katika vituo vya kizuizi vya Israeli, hali ambayo imesababisha Wapalestina kukumbwa na utapiamlo na njaa.
Wapalestina huko Gaza kwa sasa wanakabiliwa na njaa kali inayosababishwa na Israeli, huku vifo vya kila siku kutokana na utapiamlo vikiripotiwa.
“Hatuzungumzi hapa juu ya maisha ya anasa au starehe, bali ni hali za msingi za kuishi kama zinavyotakiwa kisheria,” uamuzi huo ulisema. “Tusishiriki katika mienendo ya maadui wetu wabaya zaidi.”
Jeshi la Israeli limewakamata maelfu ya Wapalestina kutoka Gaza na Ukingo wa Magharibi unaokaliwa tangu kuanza kwa vita ambavyo sasa vinaelekea kutimiza miaka miwili, na limeongeza kwa kiasi kikubwa ukamataji holela wa watu kwa tuhuma za “ugaidi”.
Wafungwa wengi waliowachiliwa wameelezea hali mbaya katika vituo vya kizuizi vya kijeshi vya Israeli, zikiwemo mateso na ukatili, njaa, ukosefu wa huduma za matibabu, msongamano, na magonjwa.
ACRI, mojawapo ya mashirika mawili yaliyowasilisha kesi hiyo, ilisema kwamba wafanyakazi wake walikumbwa na “mashambulizi ya matusi, vitisho na udhalilishaji wa maneno” kutoka kwa viongozi waandamizi wa serikali ya Israeli na wabunge wa mrengo wa kulia wakati wa kusikilizwa kwa kesi hiyo katika Mahakama ya Juu.
“Milipuko hiyo ya hasira ilianza kuonekana si kama maonyesho ya nguvu au vitisho, bali kama mlipuko wa kukata tamaa,” ilisema taarifa yao mwishoni mwa Julai, kesi hiyo ilipoanza.