Macron aanza ziara Madagascar

Jared Ombui
2 Min Read
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron.

Rais Emmanuel Macron ameanza ziara rasmi ya siku mbili nchini Madagascar, akilenga kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kudhihirisha upya uwepo wa Ufaransa katika eneo la Bahari ya Hindi, licha ya mvutano unaoendelea kuhusu masuala ya kihistoria ya ukoloni.

Hii ni mara ya kwanza kwa rais wa Ufaransa kufanya ziara rasmi nchini humo tangu Rais wa zamani Jacques Chirac alipotembelea mwaka 2005.

Madagascar, koloni la zamani la Ufaransa lililo karibu na pwani ya Msumbiji, lina umuhimu mkubwa wa kijiografia na kisiasa katika ukanda huu.

Macron na mkewe, Brigitte, walipokelewa katika uwanja wa ndege wa kimataifa na watoto waliokuwa wakipeperusha bendera za Ufaransa na Madagascar, kabla ya kuelekea jijini Antananarivo kwa mazungumzo na Rais Andry Rajoelina pamoja na viongozi wa biashara.

Katika maandalizi ya ziara hiyo, mamlaka za jiji ziliendesha kampeni ya usafi mkubwa: watu wasio na makazi waliondolewa katika maeneo ya wazi na handaki walikokuwa wakilala, huku wachuuzi wa mtaani wakitakiwa kuondoka — hatua iliyokosolewa na baadhi ya wakazi wa jiji.

“Unafiki mtupu,” alisema Feno, mwanafunzi mwenye umri wa miaka 22. “Tembea tu mitaa mitatu kutoka hapa utaona Antananarivo halisi”.

Ufaransa inatumia ziara hii kujihakikishia nafasi yake ya kimkakati katika eneo la Bahari ya Hindi, ambapo inakabiliana na ushindani unaoongezeka kutoka kwa China na Urusi. Bado kuna mivutano juu ya maeneo kadhaa, hususan visiwa vidogo ambavyo bado vinamilikiwa na Ufaransa licha ya koloni zake nyingine za Afrika kupata uhuru.

Vivyo hivyo, taifa jirani la Comoro linadai kisiwa cha Mayotte, ambacho kwa sasa ni idara ya ng’ambo ya Ufaransa.

Maeneo yote mawili yana umuhimu mkubwa wa kimkakati kwa Msumbiji — njia kuu ya biashara ya kimataifa — na yanatajwa kuwa na utajiri mkubwa wa gesi na mafuta.

Share This Article