Chama cha Walimu wa shule za sekondari na vyuo nchini – KUPPET, kimeishutumu serikali kwa kukata bajeti ya shilingi bilioni 62, za kufadhili elimu katika makadirio ya bajeti ya mwaka 2025/2026.
Akiwahutubia wanahabari jana katika makao makuu ya chama hicho, Katibu wa KUPPET Akelo Misori, alionya kuwa hatua hiyo inahatarisha ubora wa viwango vya elimu, ikiwemo mipango ya lishe shuleni, mikopo ya masomo kwa wanafunzi na kuajiriwa kwa walimu wapatao 20,000 Januari mwaka ujao.
Misori ameitaka serikali kufutilia mbali hatua hiyo na kurejeshwa kwa bajeti ,akionya kuwa uamuzi huo utasambaratisha mafanikio yaliyoafikiwa katika sekta ya elimu nchini hususan mtaala mpya wa elimu ya umilisi (CBC).