Serikali ya Kenya kupitia idara ya maswala ya ughaibuni, imetoa wito kwa raia wake wanaoishi Israel na Iran kujisajili ili wahamishwe, huku mzozo kati ya nchi hizo mbili ukiendelea.
Kwa usalama wenu na kuhakikisha tunawasaidia kunapotokea dharura yoyote, tunawahimiza kujisajili na idara ya Maswala ya ughaibuni,” ilisema wizara ya Mambo ya Nje kupitia ukurasa wa X.
Kwenye taarifa hiyo, katibu wa Maswala ya Ughaibuni Roseline Njogu , alisema serikali imewahimiza wakenya wote walio katika maeneo yenye mzozo kuwa makini zaidi na kupunguza safari zisizo za lazima.
“Usalama wa wakenya ughaibuni unasalia kuwa wa umuhimu mkubwa kwetu, huku hali katika mashariki ya kati ikiendelea kuwa mbaya,” alisema Njogu.