Jeshi la Israel limewaonya watu walio katika Jiji Kuu la Iran,Tehran kuondoka mara moja.
“Katika kipindi cha saa zijazo, IDF itafanya operesheni katika eneo hilo, kama ilivyofanya katika siku za hivi karibuni kote Tehran, kushambulia miundombinu ya kijeshi ya utawala wa Iran,” msemaji wa Jeshi la Ulinzi la Israel Avichay Adraee aliweka ujumbe huo kwenye mtandao wa X.
Aidha Adraee pia ameambatanisha ramani kwenye maeneo yaliolengwa katika onyo hilo akisema watu katika sehemu za wilaya tatu ya jiji hilo wanapaswa kuondoka.
“Uwepo wako katika eneo hili unahatarisha maisha yako,” onyo hilo linaisha hapo.
Hayo yanajiri huku watu walio magharibi mwa Tehran, walisema kwamba wamesikia milipuko mikubwa.
Video na picha zinazojitokeza kwenye mitandao ya kijamii ya Iran zinaonyesha moshi unaopanda katika milima iliyo karibu iliolengwa.
Vyombo vya habari vya Iran vimeripoti kuwa ulinzi wa anga wa mji huo umeanzishwa magharibi mwa Tehran, huku shirika la habari la Fars linaloshirikiana na IRGC likisema Israel imelenga kambi ya kijeshi katika eneo hilo.