Naibu Inspekta Jenerali wa Polisi Eliud Lagat, ametoa tahadhari dhidi ya vitendo vya uhuni wakati wa mikutano ya kisiasa na mikutano ya hadhara.
Kupitia kwa taarifa kupitia ukurasa wa X siku ya Ijumaa, Lagat, aliwaonya wanasiasa na watu binafsi wanaosajili magenge ya wahalifu, ili kusababisha fujo wakati wa mikutano huku akisema kwamba wanaohusika watashughulikiwa ipasavyo.
Lagat, ambaye alikuwa akizungumza wakati wa mkutano wa ngazi ya juu wa usalama uliowaleta pamoja maafisa wanaoongoza vituo vya polisi kote katika Kaunti ya Nairobi, alisema vitendo vya uhuni vimewaacha watu kadhaa wakiuguza majeraha, na kwamba hawatavumiliwa.
Lagat wakati huo huo alifichua kuwa huduma ya taifa ya polisi imeweka mikakati ya kukabiliana na mashambulizi ya majambazi, pamoja na kukabiliana na biashara ya pombe haramu na mihadarati katika makazi yasiyo rasmi jijini Nairobi.
Aliongeza kuwa wanakabiliana na visa vya ufisadi katika vituo vya polisi na pia kushughulikia maswala ya afya ya akili miongoni mwa maafisa wa polisi.