Gavana Guyo afanya mabadiliko serikalini

Marion Bosire
2 Min Read
Abdi Guyo, Gavana wa kaunti ya Isiolo

Gavana wa Kaunti ya Isiolo, Abdi Ibrahim Guyo, amefanya mageuzi makubwa katika serikali yake, miezi miwili tu baada ya kunusurika kufurushwa afisini kupitia jaribio la kumwondoa mamlakani.

Kupitia taarifa rasmi ya Amri ya Utendaji Nambari Moja iliyosomwa na Mratibu wa Mawasiliano wa Kaunti, Hussein Salesa, jioni ya jana, Gavana Guyo alitangaza kuwafuta kazi Mawaziri wawili wa kaunti, kumpokonya majukumu Naibu Gavana na kupunguza idadi ya Maafisa Wakuu kutoka 31 hadi 21.

Waliopoteza nyadhifa zao serikalini ni Yusuf Dahir aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Barabara, Miundombinu, Mipangilio ya Miji, Nyumba na Maendeleo ya Mijini na Ali Wario Sarite aliyekuwa Waziri wa Maji, Mazingira, Nishati, Rasilimali Asili na Mabadiliko ya Tabianchi.

Naibu Gavana, Dkt. James Lowasa, ambaye alikuwa akihudumu kama Waziri wa Elimu na Maendeleo ya Awali ya Mtoto, sasa atakuwa bila wizara yoyote rasmi.

Licha ya mabadiliko haya, Gavana Guyo hakutangaza majina mapya kujiunga na baraza lake la mawaziri, bali aliongeza majukumu kwa mawaziri waliosalia

Lucy Kaburu, Waziri wa Afya, sasa atahudumu pia kama Waziri wa Fedha na Mipango ya Kiuchumi, kufuatia kuondoka kwa Abdullahi Banticha Jaldesa aliyekuwa akishikilia nafasi hiyo na sasa ni Spika wa Bunge la Kaunti.

Lucy pia atakuwa kaimu Waziri wa Elimu, nafasi iliyotwaliwa kutoka kwa Naibu Gavana.

Dkt. Lawrence Mwongela, Waziri wa Utalii na Wanyamapori, Biashara na Uwekezaji, Ushirika, Maendeleo ya Biashara Ndogo na Usimamizi wa Utumishi wa Umma, ataongeza majukumu kama Waziri wa Maji, Mazingira, Nishati, Rasilimali Asili na Mabadiliko ya Tabianchi.

Yusuf Mohamed, Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi, sasa pia atahudumu kama Waziri wa Ardhi, Barabara, Kazi za Umma na Miundombinu, Mipangilio ya Miji, Nyumba na Maendeleo ya Mijini.

Aidha, Ali Edin Abdi ametangazwa kuwa Msemaji wa Serikali ya Kaunti ya Isiolo, akiwa wa kwanza kushikilia nafasi hiyo tangu kuanzishwa kwa serikali ya kaunti.

Hatua hizi zimechukuliwa kuwa juhudi za kuondoa wale wanaodhaniwa kuwa walihusika au kuunga mkono juhudi na njama ya kumng’oa mamlakani, na kuwatunuku wale waliobaki waaminifu kwake wakati wa msukosuko wa kisiasa.

Share This Article