Mapigano ya Thailand na Cambodia yaingia siku ya tatu

Marion Bosire
2 Min Read

Mapigano kati ya Thailand na Cambodia yameendelea kwa siku ya tatu, huku mashambulizi ya mizinga na ya anga yakiwalazimu watu zaidi ya nusu milioni kukimbia makwao na kutafuta hifadhi, kwa mujibu wa mamlaka.

Maafisa wa majirani hao wawili wa Asia ya Kusini Mashariki, Jumatano walishutumiana kwa kuanzisha tena mzozo ambao tayari umewaua angalau wanajeshi na raia 13 wiki hii.

“Zaidi ya watu 400,000 wamehamishwa na kupelekwa katika makazi salama” katika mikoa saba, msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Thailand, Surasant Kongsiri, aliambia waandishi wa habari.

“Raia wamelazimika kuhama kwa wingi kutokana na kile tulichokadiria kuwa tishio la karibu kwa usalama wao,” alisema.

Jeshi la Thailand pia liliripoti kwamba maroketi yaliyopigwa kutoka Cambodia yameanguka karibu na Hospitali ya Phanom Dong Rak katika mkoa wa Surin Jumatano asubuhi na kulazimu wagonjwa na wafanyakazi wa hospitali kujificha kwenye handaki.

Katika nchi jirani ya Cambodia watu 101,229 wamehamishwa na kupelekwa katika makazi salama na nyumba za ndugu katika mikoa mitano, kulingana na msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Cambodia, Maly Socheata.

Tovuti ya Cambodianess, inayoendeshwa na Shirika la Utangazaji la Vyombo vya Habari la Cambodia, iliripoti kwamba ndege za kivita za Thailand zilishambulia maeneo mawili nchini humo, huku mashambulizi ya mizinga ya Thailand yakiendelea katika maeneo mengine matatu.

Tovuti ya habari ya Thailand, Matichon Online, pia iliripoti kwamba jeshi la nchi hiyo limepeleka ndege kushambulia kituo kimoja cha kijeshi cha Cambodia kando ya mpaka Jumatano asubuhi.

Maroketi na mashambulizi ya mizinga ya Cambodia pia yalilenga maeneo 12 muhimu katika mikoa minne ya Thailand mapema asubuhi, kwa mujibu wa gazeti la The Nation la Thailand likinukuu vyanzo vya kijeshi.

Hakukuwa na taarifa za mara moja kuhusu vifo au majeruhi.

Share This Article