Gavana wa kaunti ya Isiolo, Abdi Guyo, amewahakikishia wakazi wa wadi za Burat na Ngaremara kuwa uongozi wa kaunti hiyo umejitolea kuutafutia suluhu mgogoro wa muda mrefu wa ardhi unaowahusisha na Jeshi la Ulinzi la Kenya (KDF).
Gavana Guyo amewataka wakazi kuwa watulivu huku viongozi waliochaguliwa wakitafuta msaada kutoka kwa Rais William Ruto ambaye pia ni Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, ili kuhakikisha wananchi hawafurushwi kwenye ardhi yao ya asili.
Akizungumza katika uwanja wa shule ya msingi ya Ngaremara wakati wa maadhimisho ya Siku ya Mashujaa, Gavana Guyo alisema kuwa serikali ya Rais Ruto imeonyesha dhamira ya dhati ya kutatua suala hilo, na hatua muhimu zilichukuliwa baada ya Rais kuagiza aliyekuwa Waziri wa Ulinzi, Aden Duale – ambaye sasa amehamishwa Wizara ya Afya – kulifuatilia suala hilo kwa haraka.
Hata hivyo, alibainisha kuwa mgogoro haujamalizwa kikamilifu kutokana na baadhi ya watu waliokwenda mahakamani kuhusu suala hilo kukataa kufutilia mbali kesi na kukubali suluhu ya nje ya mahakama.
Gavana huyo alitoa wito kwa viongozi wote waliochaguliwa kuungana na kushirikiana kwa pamoja kuhakikisha haki inapatikana kwa wananchi walioathirika.
Naye Naibu Gavana, Dkt. James Lowasa, alieleza kuwa wanajeshi wamekuwa kero kwa jamii kwa miongo mingi kwa kujaribu kuwafurusha wananchi kutoka kwenye ardhi yao ya asili, licha ya ukweli kwamba jeshi lilikuta watu hao wakiwa wamekwisha kuishi na kulima maeneo hayo kwa muda mrefu.
Alisisitiza kuwa ni wakati sasa kwa jeshi kutumia maeneo makubwa ambayo hayana makazi ya watu kwa ajili ya mazoezi yao badala ya kuwanyima raia ardhi ya uzalishaji.
Kamishna mpya wa kaunti ya Isiolo, David Kiprop, alitoa wito wa kuwepo amani na ushirikiano kati ya jamii zote za Isiolo, akieleza kuwa rasilimali zilizopo zinatosha kwa wote.
Aidha, aliwahimiza viongozi waliochaguliwa kuungana na kuhudumia wananchi, hasa baada ya jaribio la kumbandua Gavana Guyo kushindikana.