Ndege isiyo na rubani ya jeshi la Rwanda yaanguka na kusababisha majeruhi

Martin Mwanje
2 Min Read
Picha iliyovuja inaonyesha ndege isiyo na rubani ya Bayraktar TB2 iliyotengenezwa na Uturuki. Jeshi la Rwanda halikufichua aina ya ndege isiyo na rubani iliyoanguka.

Jeshi la Ulinzi la Rwanda (RDF) linasema ndege yao ndogo ya kivita isiyokuwa na rubani (drone) ilianguka Jumanne, na kuwajeruhi watu watatu katika eneo la magharibi mwa nchi.

Taarifa ya RDF ilisema kuwa “hali mbaya ya hali ya hewa” ilisababisha ndege hiyo isiyo na rubani, ambayo ilikuwa ikitumika kwa mafunzo, kwenda njiani na kuanguka katika wilaya ya Rutsiro.

RDF ilisema waliojeruhiwa ni wanafunzi watatu “waliokuwa wakirejea nyumbani kutoka shuleni”. Ilisema wawili walipelekwa katika Kituo cha Afya cha Kivumu kwa matibabu, huku wa tatu akipelekwa katika Hospitali ya Murunda – wote katika eneo moja.

RDF haikufichua aina ya ndege isiyo na rubani iliyoanguka saa 7:40 mchana.

Hii ni mara ya kwanza kwa jeshi la Rwanda kutangaza kuwa ndege yake isiyo na rubani imeanguka katika ardhi ya Rwanda.

Picha ya wavuti wa jeshi la Rwanda inaripoti kuwa mnamo Julai 2016, maafisa wa usalama walianza mafunzo ya matumizi ya ndege zisizo na rubani katika anga ya Rwanda.

RDF inasema inazihurumia familia za watoto waliojeruhiwa na inajutia “matatizo yaliyosababishwa na ajali hii.”

Jeshi la Rwanda limeongeza kuwa linafanya kazi na mamlaka za mitaa na madaktari kuhakikisha kwamba watoto katika hospitali hiyo “wanapata huduma za matibabu zinazofaa”.

RDF pia ilisema inatoa “msaada wa lazima kwa watoto na familia zao”.

TAGGED:
Share This Article