Mlanguzi akamatwa na bangi kunaswa Sotik

Marion Bosire
1 Min Read

Maafisa wa usalama kutoka Kituo cha Polisi cha Sotik wamefanikiwa kumkamata mhalifu sugu wa usafirishaji wa dawa za kulevya na kunasa kilo 350 za bangi ya thamani ya takribani shilingi milioni 7.

Wakati wa doria ya kawaida katika barabara ya kutoka Sotik kuelekea Kaplong, maafisa hao walisimamisha gari aina ya Toyota Isis lenye nambari za usajili KBT 147X kwa ukaguzi.

Hata hivyo, kwa ujasiri wa kushangaza, dereva wa gari hilo aliliacha ghafla na kukimbia kwa miguu, jambo lililozua mashaka.

Baada ya ukaguzi wa haraka wa gari hilo, maafisa waligundua magunia saba ya bangi ndani ya gari hilo. Dawa hizo za kulevya pamoja na gari hilo lililoachwa zilipelekwa mara moja katika Kituo cha Polisi cha Sotik kwa hatua zaidi.

Wakiwa na dhamira ya kumchukulia mshukiwa hatua za kisheria, wachunguzi walizindua msako mkali.

Kupitia uchunguzi wa kielektroniki, walimfuatilia mtuhumiwa, aliyetambuliwa kama Diab Asman Bhakit, hadi alipokuwa amejificha katika eneo la Kibra, kaunti ya Nairobi na hatimaye wakamkamata.

Bhakit alipelekwa katika Kituo cha Polisi cha Sotik ambapo anazuiliwa kwa sasa, akiendelea na mchakato wa uchunguzi akisubiri kufikishwa mahakamani.

TAGGED:
Share This Article