Kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong Un, amesimamia jaribio la makombora mawili mapya ya ulinzi wa anga, kwa mujibu wa taarifa ya Shirika la Habari la Korea Kaskazini (KCNA).
Taarifa hiyo ya serikali imesema kuwa silaha hizo zina “uwezo wa juu wa kivita” na zinatumia “teknolojia ya kipekee,” ingawa haikutoa maelezo ya kina kuhusu vipengele vya teknolojia hiyo.
Jaribio hilo lilitekelezwa Jumamosi na, kulingana na KCNA, “limethibitisha kuwa sifa za kiteknolojia za aina hizo mbili za makombora zinafaa sana kwa kuharibu malengo mbalimbali ya angani,” likiwemo mashambulizi kutoka kwa ndege zisizo na rubani (drones) na makombora ya mwelekeo wa chini (cruise missiles).
Hatua hiyo inajiri wakati mvutano unaongezeka katika Rasi ya Korea.
Siku chache kabla ya jaribio hilo, Korea Kusini ilifyatua risasi za onyo Jumanne dhidi ya wanajeshi wa Korea Kaskazini waliovuka kwa muda Mfereji wa Kutenganisha Kijeshi (DMZ) unaotenganisha nchi hizo mbili.
Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Yonhap, Kamandi ya Umoja wa Mataifa ilieleza kuwa karibu wanajeshi 30 wa Korea Kaskazini walivuka mpaka huo unaolindwa kwa ulinzi mkali kati ya pande hizo mbili.
Pyongyang ilijibu tukio hilo kwa kuishutumu Seoul kwa kile ilichokiita “uchokozi wa makusudi,” ikiongeza ukakasi katika uhusiano wa muda mrefu uliojaa misuguano.
Wakati huo huo, Korea Kusini na Marekani zimeendelea na mazoezi makubwa ya kijeshi ya pamoja katika eneo hilo tangu Jumatatu. Mazoezi hayo yanafanyika katika kipindi ambacho diplomasia kati ya Korea Kaskazini na Kusini inadorora, licha ya ahadi za kisiasa zilizotolewa wakati wa kampeni na Rais mpya wa Korea Kusini, Lee Jae Myung, ambaye aliahidi “kuboresha uhusiano wa pande mbili.”
Licha ya juhudi hizo, dada wa Kim Jong Un amezipinga vikali, akizitaja kuwa ni za hila na zisizo na dhati.
Hili limeifanya hali ya kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili kuwa tete zaidi.
Korea Kaskazini na Korea Kusini zimegawanyika tangu kumalizika kwa Vita vya Korea mwaka 1953.
Ingawa vita hivyo vilikoma kwa kusainiwa kwa makubaliano ya kusitisha mapigano, hakuna mkataba rasmi wa amani uliowahi kutiwa saini, jambo ambalo limeacha nchi hizo mbili zikiwa bado “kihalali katika hali ya vita,” licha ya kwamba hakuna mashambulizi ya moja kwa moja yaliyotokea kwa miaka mingi.