Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Miji Alice Wahome, amepuuzilia mbali uvumi unaoenezwa mitandaoni kwamba anapanga kujiuzulu.
Akizungumza wakati wa zoezi la upanzi miti katika kaunti ya Laikipia, Wahome alisisitiza kuwa nafasi yake katika serikali ya Kenya Kwanza iko imara kwa sababu ya utendakazi wake.
“Baada ya baadhi ya watu kuondolewa, wengine walianza kuandika kuwa hata Alice Wahome ataondoka. Hizo ni ndoto za mchana. Siwezi kujiuzulu kutoka kwa serikali ambayo nilipigania kwa nguvu kuianzisha,” alisema Wahome.
“Wale waliotolewa hawakuwa wakifanya kazi. Mimi nafanya kazi, na kazi nzuri ndiyo inayomweka mtu kazini,” aliongeza Waziri huyo.
Waziri huyo aliyasema hayo Ijumaa wakati alipowaongoza wakazi wa eneo la Mutitu, katika msitu wa Uaso Narok, Nyahururu, kushiriki zoezi la kila mwezi la upanzi wa miti. Mawaziri wa serikali wamepangiwa kusimamia zoezi hilo katika angalau kaunti mbili kila mmoja, kama sehemu ya mpango wa taifa wa kupanda miti bilioni 15 katika kipindi cha miaka 10.
Alitaja mafanikio ya serikali ya Rais William Ruto, kama vile kumaliza wimbi la uhalifu na uporaji Laikipia, kuwa sababu ya kumuunga mkono rais huyo. Alitoa wito kwa wakazi wa Laikipia kuwachagua viongozi kwa misingi ya utendaji, si kwa upendeleo wa kisiasa.
“Msifikirie mtu wenu mnapoenda kwenye uchaguzi. Chagueni mtu atakayewatumikia kwa bidii,” alihimiza. Pia aliwashauri kuepuka kujiingiza mapema kwenye siasa za uchaguzi kwani hiyo inaweza kuvuruga maendeleo.
Wahome alieleza kuwa anaunga mkono kurejeshwa kwa mfumo wa shamba, ambao unaruhusu wananchi kulima mazao ya chakula pamoja na miche ya miti katika maeneo ya misitu kwa muda fulani.
Alisema hatua hiyo itasaidia kuhakikisha miche inatunzwa vizuri na kuongeza kiwango cha miti inayoendelea kukua.
“Nimekubaliana na Waziri wa Mazingira kuhusu kuanzisha mfumo wa shamba katika Laikipia na tunasubiri idhini rasmi kutoka kwa Msimamizi Mkuu wa Misitu,” alisema. “Hii ni njia bora ya kuwahusisha wananchi katika kufanikisha lengo la miti bilioni 15, huku wakiboresha maisha yao.”
Waziri Wahome na Gavana wa Laikipia, Joshua Irungu, waliitaka Mamlaka ya Huduma za Misitu (KFS) kuhakikisha wanatoa miche ya miti ya matunda kwa ajili ya awamu ijayo ya upandaji miti. Miche hiyo itagawiwa kwa wananchi kupandwa majumbani mwao.
Wahome alisema hadi sasa miche 80,000 ya miti imepandwa katika Kaunti ya Laikipia tangu kuzinduliwa kwa mpango huo wa kitaifa. Gavana Irungu alisema upandaji wa miti ya matunda na kahawa utasaidia kufanikisha lengo la kupanda miti milioni 340 katika kaunti hiyo katika kipindi cha miaka 10.