Eliud Owalo ambaye ni naibu mkuu wa wafanyakazi katika afisi ya Rais anayesimamia utendaji na uwasilishaji, amekubali rasmi wadhifa wake kama naibu mlinzi wa timu ya soka ya Gor Mahia.
Alichukua hatua hiyo katika hafla ya kipekee iliyoandaliwa katika hoteli ya Hermosa jijini Nairobi na ambayo ilihudhuriwa na wasimamizi wa klabu hiyo ya soka, wataalamu wa kiufundi na wachezaji.
Owalo ambaye aliwahi kuhudumu kama waziri wa mawasiliano na uchumi dijitali, anachukua wadhifa huo kutoka kwa Cyprian Otieno Awiti, ambaye alijiondoa kutokana na matatizo ya kiafya.
“Tunashukuru sana kwa kujitolea, shauku na huduma ambayo Gavana Awiti alitoa wakati akihudumu katika wadhifa huu.” Alisema Owalo katika taarifa.
Aliongeza kusema kwamba japo Awiti amejiondoa, wanatizamia usaidizi na maelekezo kutoka kwake watakapohitaji.
Owalo amesema kama naibu mlinzi wa Gor Mahia, wajibu wake ni Kubuni upya, kufufua na kuhuisha tena mipango ya timu ya Gor Mahia akiwa na maono ya kuibadilisha kuwa taasisi kubwa na iliyofanikiwa ya soka barani Afrika.
Vipaumbele kulingana naye ni pamoja na maendeleo ya miundombinu ambapo analenga kuongoza ujenzi wa uwanja wa kisasa pamoja na jumba la timu na nyumba za wachezaji na wahudumu wengine wa timu.
Alitaja mipango mingine kama utaalamishaji, mipango ya kimkakati, usajili wa wachezaji, utawala bora, ubora wa mchezo, maslahi ya wachezaji, usajili wa wanachama zaidi na mauzo.
Waliohudhuria hafla ya leo ni pamoja na mwenyekiti wa Gor Mahia Ambrose Rachier, naibu mwenyekiti Sally Bollo, katibu mkuu Nicholas Arum na mwekahazina wa heshima Gerphas Okuku.