Watu zaidi ya 50 wafariki kwenye ajali Guatemala

Tom Mathinji
1 Min Read
Zaidi ya watu 50 wafariki kwenye ajali Guatemala

Watu zaidi ya 50 wamefariki baada ya basi walimokuwa wakisafiria kuanguka kutoka kwenye daraja katika jiji la Guatemala, maafisa wa zimamoto wamesema.

Basi hilo, lililokuwa likielekea mji mkuu kutoka idara ya El Progreso, lilikuwa na abiria 75, na lilianguka chini ya bonde lenye urefu wa mita kadhaa na kutumbukia kwenye mfereji wa maji taka, kulingana na idara ya zimamoto ya eneo hilo.

Miongoni mwa waliofariki ni watoto wadogo.

Miili ya wengi kati ya 54 waliofariki, akiwemo dereva wa basi, iko katika chumba cha kuhifadhi maiti cha muda karibu na eneo la ajali, kwa mujibu wa maafisa wa zimamoto.

Huduma za dharura zilisema takriban watu wengine 15 waliokolewa wakiwa na majeraha mabaya, ingawa idadi kamili ya walionusurika haijulikani.

Picha zilizosambazwa kwenye mitandao ya kijamii zinaonyesha ukubwa wa ajali hiyo, huku basi hilo likipinduka na waokoaji wakiondoa miili ya marehemu na walionusurika.

Taratibu za kutambua miili hiyo zimeanza na mamlaka imeanza kuandaa orodha za majina ya marehemu.

TAGGED:
Share This Article