Waandalizi wa makala ya 17 ya fainali za kuwania kombe la bara Ulaya Ujerumani, wamefuzu kwa hatua ya mwondoano baada ya kusajili ushindi wa pili kundini A Jumatano usiku walipowaadhibu Hungary mabao 2 kwa bila.
Jamal Musiala na nahodha İlkay Gündoğan walifunga dakika za 22 na 67 mtawalia kuwapa mabingwa hao mara tatu ushindi uliowafuzisha kwa raundi ya pili wakiwa na pointi sita.
Kwenye mtanange mwingine wa kundi A, Scotland na Uswizi walitoshana nguvu ya bao moja kwa moja uwanjani RheinEnergie.
Scott McTominay aliiweka Scotland mbele kunako dakika ya 13 kisha Xherdan Shaqiri akakomboa dakika ya 26.
Kundini B Croatia yake Luka Modric ilitoka sare ya mabao 2 dhidi ya Albania.
Croatia na Albania zilipoteza mechi za mwanzo dhidi ya Uhispania na Italia mtawalia na ambazo zitamenyana leo saa nne usiku.
Mechi nyngine za leo saa kumi jioni na saa moja usiku ni za kundi C.
Slovenia watazichapa dhidi ya Serbia kisha Denmark wakabane koo na Uingereza.