Watu wapatao 78 wamethibitishwa kufariki na wengine 41 hawajulikani waliko kufuatia mafuriko ya ghafla katikati mwa Texas, nchini Marekani.
Eneo lililoathirika zaidi ni Kaunti ya Kerr, ambako vifo 68 vimeripotiwa, wakiwemo watoto 28 kwa mujibu wa maafisa wa dharura. Idadi ya vifo inatarajiwa kuongezeka, kwani dhoruba zaidi zinatarajiwa katika muda wa saa 48 zijazo.
Wahudumu wa uokoaji wanakabiliana na mazingira hatari, ikiwa ni pamoja na tope, mabaki ya majengo na nyoka wenye sumu, wakati shughuli ya kutafuta manusura inabadilika kuwa ya kurejea na miili.
Mkazo mkubwa umeelekezwa katika Kambi ya Mystic, iliyo kando ya Mto Guadalupe, ambako maji yalizidi kambi hiyo kabla ya alfajiri.
Miongoni mwa waliofariki ni wakazi wa kambi hiyo na mkurugenzi wa muda mrefu wa kambi hiyo, Richard Eastland. Wasichana kumi na mshauri mmoja wa kambi hiyo bado hawajapatikana.
Gavana wa Texas Greg Abbott, alizuru eneo hilo Jumamosi, alieleza hali hiyo kuwa ya kutisha kabisa na akaahidi kwamba mamlaka hazitasita kufanya kila juhudi kupata waliopotea.
Mafuriko hayo, yaliyosababishwa na kuongezeka ghafla kwa maji ya mto kwa futi 26 ndani ya dakika 45 pekee, yameacha uharibifu mkubwa.
Nyumba na barabara karibu na Kerrville zimeharibiwa vibaya na mabaki, miti iliyopinduliwa na nyaya za umeme zilizokatika zimeenea kote katika eneo hilo.
Rais Donald Trump ametangaza janga kubwa kwa Kaunti ya Kerr, jambo lililowezesha msaada wa shirikisho kuanza kutolewa. Anatarajiwa kuzuru Texas baadaye wiki hii.