Mwanamuziki wa Nigeria Innocent Idibia maarufu kama 2Baba au 2Face Idibia ametangaza kwamba amebadilisha usimamizi wake katika hatua ya kustawisha kazi zake.
Usimamizi huo mpya ambao ni kampuni kwa jina “A Guy Entertainment” ulitoa taarifa rasmi kuhusu hatua hiyo inayochukuliwa kuwa kubwa katika maisha ya msanii huyo.
Hatua hii inaashiria mwelekeo mpya na wa kishujaa unaolenga kufufua na kupanua urithi wake katika tasnia ya burudani ya Afrika inayoendelea kubadilika.
Akiwa na uzoefu wa zaidi ya miaka 30 katika muziki, 2BABA anatambuliwa sana kama mwasisi wa muziki wa Afro-pop na sauti yenye ushawishi mkubwa kwa mabadiliko ya kijamii kote barani.
Timu mpya iliyoteuliwa, ambayo inajumuisha wataalamu katika biashara ya muziki, chapa, ubunifu wa kidijitali, na sheria ya burudani, itasimamia kila nyanja ya taaluma yake, kuanzia maandalizi ya muziki na ushirikiano wa kimataifa hadi kampeni za kijamii zenye athari.
“Nina furaha kuhusu sura hii mpya. Mabadiliko ni sehemu muhimu ya ukuaji na ninaamini timu hii inaelewa maono yangu, urithi wangu, na tunakoelekea. Hatuishii tu kusherehekea yaliyopita tunaunda uchawi zaidi”2BABA alisema.
Mashabiki wanatarajia miradi mipya, maonyesho ya moja kwa moja na ushirikiano wa ubunifu katika miezi ijayo, yote yakiwa yamejengwa juu ya maadili ya msingi yanayobeba ushawishi wa kudumu wa 2BABA: uhalisia, ubora, na uwajibikaji wa kijamii.